Involvement

Nakusifia

(Picha kwa hisani ya WBUR)

Na Abdul Shaban

Mke ninakusifia,
Mzuri umetulia,
Na wala sitojutia,
Kifua nakitanua.

Nakupongeza kwa hili,
Nyumbani nikiwasili,
Moyo wangu huwa tuli,
Hali unanijulia.

Nilipanga mikakakati,
Masijidi nikaketi,
Dua pia na swalati,
Nikamuomba jalia.

Nikataraji mazuri,
Mwenye dini ndo mzuri,
Mola akanitabiri,
Wewe ndo ukanijia.

Sitara unatimiza,
Mazuri wanihimiza,
Kikosea wanijuza,
Toba nije kutubia.

Wanihimiza kwakweli,
Nichume yalo halali,
Adhabu zake Jalali,
Kwangu unanihofia.

Hongera we mke wangu,
Wanilelea wanangu,
Malezi yaso machungu,
Mola wao kumjua.

Naomba kwake manani,
Tusitengane ndoani,
Wenye shari maishani,
Wacheze pata potea.

Zimekujaa swifati,
Mahabuba habibati,
Nitazimaliza beti,
Sifa hazitoishia.

Utenzi naumaliza,
Machozi nabubujiza,
Nikimuomba muweza,
Amani kutujalia.

Hapa sasa ndo kikomo,
Hilo ndilo langu Somo,
Sitoufunga mdomo,
Nitazidi kusifia.

Leave a Comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Scroll to Top