Involvement

Matokeo ya Ligi kuu Nchini Uingereza

Na Denni Mungai

Manchester City walipata ushindi wa mabao mawili kwa moja dhidi ya Brighton siku ya Jumamosi. Julian Alvarez alifunga bao la kwanza naye Erling Haaland alifunga bao lake la tisa msimu huu kuipa City uongozi katika kipindi cha kwanza. Ansu Fati alifunga bao lake la kwanza kama mchezaji wa Brighton lakini haikutosha kupata alama katika uwanja wa Etihad.

Katika mechi nyingine, Brentford waliipiga Burnley 3-0, Newcastle kuiduwaza Crystal Palace 4-0 nayo Wolves kupata ushindi wa karibu wa mabao mawili kwa moja dhidi ya Bournemouth. Mechi kubwa ya wikendi kati ya Chelsea na Arsenal iliisha sare ya mabao mawili. Chelsea ilikua inaongoza kwa mabao mawili lakini Declan Rice na Leandro Trossard walisawazisha na kusaidia timu yao kunyakua alama moja. Vijana wa Arteta bado hawajashindwa kutoka msimu uanze na wana alama 21 baada ya mechi tisa.

Man United waliipiku Sheffield United 2-1, mabao ya United yakifungwa na Mctominay na Diogo Dalot. Mohamed Salah alifunga mabao mawili na kusaidia timu ya Liverpool kushinda Everton 2-0 katika mechi ya kwanza siku ya Jumamosi. Siku ya Jumapili, Aston Villa waliigaragaza West Ham 4-1. Douglas Luiz alifunga mabao mawili huku Ollie Watkins akifunga bao lake la tano msimu huu. Leon Bailey alitia kimiani bao la nne na kusaidia Villa kupanda mpaka nafasi ya tano katika jedwali.

Tottenham Hotspurs walirudi kileleni mwa jedwali baada ya kuishinda Fulham 2-0. Son Heung-Min na James Maddison waliifungia timu yao na kuiipa alama tatu. Spurs wana alama mbili zaidi ya Man City, walio katika nafasi ya pili. Timu ya Postecoglou wana nafasi ya kuzidisha pengo hilo watakapocheza na Crystal Palace siku ya Ijumaa.

 

Leave a Comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Scroll to Top