Involvement

SAFARI YA UMAUTI

Na Abdul Shaban

 

Maradhi yamenisibu, hadi leo naugua,

Sasa naona aibu, afya imenipotea,

Naomba kwake Wahabu, kwa rehema za jalia,

Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

 

Naumwa nakondeana, dawa haziwezi tibu,

Na kula siwezi tena, ameshasema tabibu,

Ndugu wanawaza sana, waketi nami karibu,

Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

 

Nikitizama kushoto, kisha narudi kulia,

Baba lamtoka jasho, mama naye analia,

Kauli ni changamoto, kinywani imepotea,

Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

 

Muda unakaribia, kwa dalili nilo nazo,

Mauti yanifikia, hilo halina vikwazo,

Naona amenijia, asohitaji mawazo,

Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

 

Sakaratil mauti, nilikuwa nasikia,

Kiu ndo hakikauki, hata maji ya dunia,

Makosa hayajifuti, madogo nilodhania,

Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

 

Siwezi tena kutubu, kwa makosa nilofanya,

Nimekuwa kama bubu, kwa uzito wake kinywa,

Mauti yaniadhibu, na roho ninapokonywa,

Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

 

Taarifa zatolewa, wengi wanahuzunika,

*”Kweli tumeondokewa,na mpendwa bila shaka”*

Kitandani natolewa, uchafu unanitoka,

Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

 

Ndugu zangu na rafiki, wote wanalialia,

Na wengine wameketi, eti wananiombea,

Du’a zao hazifiki, natamani waambia,

Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

 

Wanatafutwa wajuzi, tayari kuandaliwa,

Wanikosha kwa simanzi, na marashi kufushiwa,

Tayari mekwisha kazi, nje sasa natolewa,

Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

 

Simanzi imegubika, baada ya kutolewa,

Madeni kutangazika, nadai na kudaiwa,

Swafu witri zimefika, ninaanza kuswaliwa,

Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

 

Mbiombio napelekwa, kaburini kufukiwa,

Tayari nimeshazikwa, huku watu wahusiwa,

Mimi nimeshachafukwa, kwa maswali ninopewa,

Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

 

 

Tubuni tubuni jama, kaburi lina vituko,

Hapa mbavu zimebanwa, natamani rudi huko,

Walau kwa moja jema, muda tena ndo haupo,

Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

 

Nashauri walimwengu, tupunguzeni machafu,

Na tuweni wachamungu, tusimuudhi Raufu,

Pepo pahala pa mungu, hawapelekwi wachafu,

Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

 

Wanadamu jihadhari, tusije kuangamia,

Tusifanye ya khatari, mola atuangalia,

Tuiandae safari, mema tukisubiria,

Kifo ni njia ya haki, safari yake lazima.

 

Leave a Comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Scroll to Top