Involvement

MTIMA WANGU WAUMA

(Picha kwa hisani ya Pinterest)

Na Abdul Shaban

 

Mwenye hisani ni nani, kwanza ninawauliza,

Aeleke mtimani, bila hata ya kuwaza,

Khatari imesheheni, yupo aloniumiza,

Mtima wangu wauma, nani aje kunipoza.

 

Tangazo nilolitoa, makusudio ninayo,

Sitaki tena madoa, asije kufata nyayo,

Awe mtuvu kapoa, atulize nilo nayo,

Mtima wangu wauma, nani aje kunipoza.

 

Ilio kubwa sababu, sasa nakwenda kusema,

Moyo aliusulubu, hakunielewa vyema,

Amri zake wahabu, hakutekeleza hima,

Mtima wangu wauma, nani aje kunipoza.

 

Mapenzi aliyapata, nami yake nilipata,

Yani alikula bata, vijana wanavyoita,

Uzuri wa kumemeta, kwa hayo mi sikujuta,

Mtima wangu wauma, nani aje kunipoza.

 

Alinikata kauli, usiku hata mchana,

Niliposema tuswali, hapo yeye alinuna,

Niliudhika kwakweli, japo nampenda sana,

Mtima wangu wauma, nani aje kunipoza.

 

Wala sikumdekeza, onyo nikampatia,

Hapa nitakufukuza, kama ukiendelea,

Hakutaka kusikiza, nikawa na mbili njia,

Mtima wangu wauma, nani aje kunipoza.

 

Apendezea uzuri, ila nikajawa khofu,

Kama kuswali khiyari, vipi niwe mkunjufu,

Nahitaji yenye kheri, toka kwa mola Raufu,

Mtima wangu wauma, nani aje kunipoza.

 

Nikafanya maamuzi, yalopendeza kwa mola,

Nikaitoa simanzi, na shetwani mwenye hila,

Tamko lenye majonzi, nakuacha kisa swala,

Mtima wangu wauma, nani aje kunipoza.

 

Gumzo likaenea, familia na mitaani,

Naye akajiendea, kurudi kwao nyumbani,

Sitaki kuteketea, kwa ghadhabu za manani,

Mtima wangu wauma, nani aje kunipoza.

 

Ukweli nishausema, hayo ndiyo yalojiri,

Nahitaji mke mwema, kwenye dini yu hodari,

Nimefika qadetama, nawaageni kwaheri,

Mtima wangu wauma, nataka wa kunipoza.

 

 

 

Leave a Comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Scroll to Top